Baada ya siku kadhaa za maandamano ya vijana nchini Nigeria huku wakiongozwa na wasanii maarufu kushinikiza kuvunjwa kwa kilichokuwa Kikosi Maalumu cha Kuzuia Wizi (Special Anti-Robbery Squad maarufu kama SARS), Mkuu wa Jeshi la Polisi wa Nigeria, Mohammed Adamu, ametangaza rasmi kuvunjwa kwa kikosi hiko.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Nigeria, Mohammed Adamu.

SARS, ambacho kilikuwa kitengo maalumu chini ya jeshi la polisi la shirikisho la Nigeria toka mwaka 1992, kwa muda mrefu kimekuwa kikilaumiwa kwa unyanyasaji, ukamataji pasipo kufuata sheria, utesaji na hata mauaji.

Maandamano ya sasa yakichagizwa na wasanii wakubwa wa muziki nchini Nigeria kama Davido, Falz, na Runtown, yalizuka baada ya video moja kusambaa ikiwaonyesha askari wa SARS wakimpiga risasi hadi kumuua raia mmoja wa kiume katika jimbo la Delta ya Kusini.

Wasanii wa Nigeria, Falz na Runtown wakishiriki maandamano ya vijana kupinga unyanyasaji wa Polisi.

Davido aliandika kwenye mtandao wa Twitter juu ya mkutano wake na IGP, Mohammed Adamu.

Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria, alitoa amri ya kuvunjwa kwa kikosi hicho baada ya kukutana na Mkuu huyo wa jeshi la polisi la nchi hiyo.

Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria alipokutana na IGP wa Nigeria, Mohammed Adamu.

Wakati hayo yakitokea nchini Nigeria, ambapo wasanii maarufu pamoja na vijana mbalimbali walipoamua kufanya maandamano dhidi ya serikali na jeshi la Polisi la nchi hiyo, nchini Tanzania hali ni tofauti kabisa kutokana na wasanii wote wakubwa kuwa bega kwa bega wakishirikiana na chama tawala kinachoongozwa na Mh. Rais John Magufuli.

Wasanii wengi wa Tanzania, kama Diamond Platnumz, Alikiba, Harmonize, na Nandy ambao hivi sasa wanazunguka sehemu mbalimbali za nchi kunadi sera za CCM na huku wakimpigia kampeni kwa kutoa burudani za bure kwa wananchi ili Rais Magufuli aweze kuchaguliwa tena kwa miaka mingine mitano.

Msanii maarufu wa Tanzania Diamond Platnumz akivalishwa kofia na Rais Magufuli wakati wa Mkutano wa kampeni.
Msanii wa Tanzania, Alikiba nae alipewa heshima ya kuvalishwa kofia na Rais Magufuli.
Harmonize anaonekana akifurahi kuvalishwa kofia na Rais Magufuli baada ya kutoa burudani ya bure kwa waliofika kwenye mkutano huo wa kampeni.

Lipo pia kundi dogo la wasanii ambao wamekuwa wakiunga mkono vyama vya upinzani lakini idadi yao na umaarufu wao sio sawa na wale wanaounga mkono Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani nchini Tanzania utafanyika siku ya tarehe 28 Oktoba, 2020 ambapo Rais Magufuli ameomba tena ridhaa ya Watanzania kuendelea kuongoza kwa miaka mingine mitano. Chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania cha CHADEMA kimemsimamisha Tundu Lissu kama mgombea wake.

Previous articleTanzania Repressing Opponents as Election Looms: Amnesty
Next articleUganda Presidential Hopeful Bobi Wine Says Security Forces Raided His Office