
Rais wa Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mhe. Freeman Aikaeli Mbowe.

Mazungumzo hayo ambayo yamefanyika Ikulu jijini Dar Es Salaam, yametokea masaa machache baada ya mwenyekiti huyo wa Chadema kuachiwa huru kutoka gerezani.

Taarifa iliyotolewa na kurugenzi ya mawasiliano ya Ikulu, ilisema, mazungumzo hayo yalilenga kuleta ushirikiano zaidi kati ya serikali na vyama vya upinzani.
Taarifa hiyo ya Ikulu inaeleza kuwa Rais Samia amezungumzia kuhusu umuhimu wa kushirikiana ili kujenga Tanzania kwa kuaminiana na kuheshimiana kwa misingi ya haki.

Kwa upande wake Mbowe amemshukuru Rais Samia kwa kuonyesha kujali huku akikubali kuwa msingi mkubwa wa kujenga Tanzania ni kusimama katika kutenda haki.
Katika taarifa hiyo, Mbowe amenukuliwa akisema kuwa wamekubaliana kufanya siasa za kistaarabu na kiungwana na kwamba yupo tayari kushirikana na Serikali kuleta maendeleo.